Serikali imezindua mpango mkubwa wa kuimarisha sekta ya burudani na michezo nchini kwa kutenga zaidi ya Shilingi bilioni 400 kwa ajili ya ujenzi wa ukumbi wa kisasa wa michezo na burudani (Arena) pamoja na studio kubwa za kisasa za utengenezaji wa filamu. Hatua hii imetangazwa na Naibu Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Mheshimiwa Hamis Mwinjuma maarufu kama Mwana FA, akisisitiza kuwa mradi huo utafungua ukurasa mpya kwa wadau wa sanaa na michezo hapa nchini.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Arena hiyo itajengwa mkoani Dodoma na itaambatana na miundombinu ya kisasa ya studio zitakazowezesha utengenezaji wa kazi za filamu zenye ubora wa kimataifa. Lengo kuu ni kuinua kiwango cha tasnia ya filamu nchini ili iweze kushindana katika soko la kimataifa pamoja na kuvutia uwekezaji zaidi.
Mradi huu unatarajiwa kuwa chachu ya maendeleo katika uchumi wa ubunifu, huku ukifungua fursa nyingi za ajira kwa vijana, kukuza vipaji vya ndani, na kuimarisha sekta ya sanaa, habari na michezo nchini Tanzania.
